Ifuatayo
ni sehemu ya bajeti ya wizara ya uchukuzi kwa upande wa usafiri na
uchukuzi kwa njia ya anga kwa mwaka 2017/2018 kama ilivyowasilishwa na
waziri Profesa Makame Mbarawa katika bunge la bajeti mjini Dodoma.
USAFIRI NA UCHUKUZI KWA NJIA YA ANGA
Udhibiti wa Usalama wa Usafiri wa Anga
154.Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuzingatia vigezo na kanuni za
usalama wa usafiri wa anga kama inavyoshauriwa na Shirika la Usafiri wa Anga
Duniani (The International Civil Aviation Organisation-ICAO). Kwa lengo la
kuimarisha na kuboresha huduma za usafiri wa anga nchini. Wizara kupitia
Mamlaka ya Usafiri wa Anga (TCAA) imeendelea kusajili ndege kulingana na
masharti ya usajili ambapo katika kipindi cha Julai 2016 hadi Machi, 2017,
ndege 14 zilisajiliwa kwa mara ya kwanza hapa nchini na ndege 79 zilikaguliwa
na kupewa vyeti vya ubora wa kuendelea kufanya kazi. Lengo ni kuhakikisha
utekelezaji wa sheria na kanuni za Usalama wa Usafiri wa Anga zinafuatwa.
155.Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia TCAA imeendelea kudhibiti ajali za
vyombo vya usafiri wa anga. Katika mwaka 2016/2017, hakuna ajali ya usafiri wa
anga iliyotokea isipokuwa yalikuwepo matukio saba (7) ya vyombo vya usafiri wa
anga. Aidha, Mamlaka imeendelea kuimarisha usalama katika viwanja vyote vya
ndege ili kuhakikisha kwamba viwanja hivyo havitumiki katika matukio ya uhalifu
yakiwemo ya kupitisha madawa ya kulevya na nyara za Umma. Pia, Mamlaka
imeendelea kuhakikisha kwamba maafisa wa usalama katika viwanja vya ndege
wanapatiwa mafunzo stahiki na kupewa leseni. Katika kipindi cha Julai, 2016 hadi
Machi, 2017, jumla ya maafisa usalama 35 walipatiwa mafunzo. Kati yao, maafisa
25 walihitimu na kupewa leseni.
156.Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2016/2017, Mamlaka ya Usafiri wa Anga
iliendelea kufanya kaguzi za viwanja vyote vya ndege nchini ili kuhakikisha
kuwa viwanja hivi vinakidhi vigezo, masharti na kanuni zilizowekwa na Mamlaka.
Viwanja vya ndege vilivyokaguliwa na kupewa vyeti vya ubora baada ya kukidhi
vigezo vya kimataifa kwa ajili ya kupokea ndege kubwa ni pamoja na Julius
Nyerere, Amani Abedi Karume na Kilimanjaro. Aidha, uimarishaji na uboreshaji wa
viwanja vya ndege vya Pemba, Geita, Matemanga na Jengo la Tatu la Abiria katika
kiwanja cha Julius Nyerere uliendelea kudhibitiwa ili kukidhi viwango vya
usalama.
157.Mheshimiwa Spika, Ili kudhibiti na kuimarisha usalama wa usafiri wa
anga nchini, TCAA inatarajia kununua rada 4 za kuongozea ndege za kiraia.
Majadiliano ya mkataba baina ya TCAA na Mkandarasi (M/s Thares Air Systems)
kutoka Ufaransa yanakamilishwa na mkataba unatarajiwa kusainiwa wakati wowote.
Rada hizi ambazo zitakamilika usimikaji wake Aprili, 2018 zitafungwa katika
viwanja vya ndege vya JNIA, Mwanza, Kilimanjaro na Songwe kwa gharama ya
Shilingi bilioni 61.3.
158.Mheshimiwa Spika, utendaji wa sekta ya usafiri wa anga nchini
umeendelea kukua. Katika mwaka 2016/2017, idadi ya abiria wanaotumia usafiri wa
anga imefikia abiria 5,057,180 ikilinganishwa na abiria 4,861,277 waliosafiri
mwaka 2015/2016. Hili ni ongezeko la asilimia 4. Kwa abiria wanaosafiri kwenda
na kutoka nje ya nchi, katika mwaka 2016/2017, jumla ya abiria 2,238,653
wanatarajiwa kusafiri ikilinganishwa na abiria 2,146,360 waliosafiri katika
mwaka 2015/2016. Sababu za ongezeko hili ni pamoja na kusainiwa kwa mikataba ya
usafiri wa anga kati ya Tanzania na nchi zingine (Bilateral Air Services
Agreements - BASA); uimarishaji wa miundombinu na huduma za viwanja vya ndege;
uboreshaji wa uwanja wa ndege wa Julius Nyerere (JNIA); ukuaji wa uchumi na
shughuli za utalii nchini. Aidha, idadi ya abiria waliosafiri ndani ya nchi
imeongezeka kutoka abiria 2,910,820 mwaka 2015/2016 hadi abiria 3,056,361
katika mwaka 2016/2017. Hii ni sawa na ongezeko la asilimia 5. Sababu ya
ongezeko la abiria wa ndani ni pamoja Serikali kutekeleza azma yake ya
kuimarisha na kuendeleza Kampuni ya Ndege Tanzania, kukua kwa shughuli za
kiuchumi, kuongezeka kwa utalii nchini na kuanzishwa kwa safari za ndege katika
maeneo mapya ya Dodoma, Bukoba na Songea.
159.Mheshimiwa Spika, utoaji wa huduma za kusafirisha mizigo katika viwanja
mbalimbali vya ndege nchini umeendelea kukua. Hadi Aprili, 2017, mizigo ya
kwenda na kutoka nchini ilifikia tani 32,773.6 kutoka tani 31,425.2
zilizosafirishwa katika kipindi kama hicho mwaka 2015/2016. Hii ni sawa na
ongezeko la asilimia 4.3. Ongezeko hili lilichangiwa na kukua kwa shughuli za
kibiashara na kiuchumi ndani na nje ya nchi na jitihada za kuboresha
miundombinu ya huduma za usafirishaji wa mizigo kupitia usafiri wa anga.
160.Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha Julai, 2016 hadi Machi, 2017,
jumla ya kampuni 59 zilipewa leseni kwa ajili ya kutoa huduma mbalimbali katika
viwanja vya ndege. Kati ya hizo, Kampuni 25 zilipewa leseni ya kutoa huduma
mbalimbali kwa kampuni nyingine za ndege (Third Party Ground Handling Services
Providers); Kampuni 14 kutoa huduma kwenye ndege zake zenyewe (self handling);
Kampuni 8 kutoa huduma za vyakula kwa kampuni za ndege na Kampuni 12 kutoa
huduma ya ugavi wa mafuta ya ndege. Aidha, hadi Machi, 2017, jumla ya kampuni
za usafiri wa ndege 61 zilikuwa zinatoa huduma za usafiri wa anga wa ratiba
(scheduled) na usiokuwa wa ratiba (non-scheduled air services). Hii ni sawa na
ongezeko la asilimia 5 ikilinganishwa na kipindi kama hicho katika mwaka
2015/2016.
161.Mheshimiwa Spika, Tanzania imeendelea kuingia makubaliano ya huduma za
usafiri wa anga na nchi mbalimbali (BASA) kwa lengo la kukidhi mahitaji ya soko
na kurahisisha usafiri katika sekta hii muhimu. Katika kipindi cha Julai, 2016
hadi Aprili, 2017, jumla ya makubaliano mapya kumi (10) yaliingiwa baina ya
Tanzania na nchi za Israel, Ureno, Guyana, Canada, Norway, Sweden, Morocco,
Falme za nchi za Kiarabu, Denmark na Uganda. Aidha, mikataba ya nchi nne (4) za
Malawi, Kenya, Oman na Uturuki ilipitiwa upya. Makubaliano haya yanafanya hadi
Aprili, 2017, Tanzania kuwa imeingia mikataba ya BASA na jumla ya nchi 68
ikilinganishwa na nchi 60 zilizokuwa zimesaini makubaliano hayo mwaka
2015/2016. Hadi Aprili, 2017, Mashirika ya ndege ya kimataifa ya ndani na nje
ya nchi 29 yalikuwa yanatoa huduma za usafiri wa anga kwa utaratibu wa BASA.
Aidha, safari za ndege kati ya nchi hizo na Tanzania zilikuwa 193 kwa juma.
162.Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kuhakikisha kuwa gharama za
mawasiliano ya ndege kati ya kituo na kituo zinapungua na zinakuwa za uhakika.
Moja ya uboreshaji huo ni kubadilisha mfumo wa mawasiliano ya anga kutoka mfumo
unaotumika sasa wa analojia kwenda mfumo wa digitali. Kazi ya kuboresha
mawasiliano kati ya waongoza ndege na marubani wakiwa angani (VHF area cover
relay station) huko Lokisale, Arusha na Changarawe, Iringa zimekamilika. Aidha,
zabuni ya kuboresha mfumo wa mawasiliano kwenda mfumo wa digitali wa
ufuatiliaji wa safari za ndege katika kituo cha Pemba ilitangazwa Februari,
2017.
Kuhusu
kufanya ukarabati wa mnara wa kuongozea ndege katika kituo cha Pemba, zabuni ya
kumpata mkandarasi wa kufanya ukarabati wa mnara huo zilifunguliwa tarehe 2
Februari, 2017. Kazi za ukarabati zinaendelea na zinatarajiwa kukamilika Juni,
2017.
163. Mheshimiwa Spika, kuhusu mfuko wa mafunzo kwa marubani na wahandisi wa
ndege, Mamlaka ya TCAA inaendelea na juhudi za kutafuta fedha ili kuweza
kufadhili wanafunzi wengi zaidi kwenye mafunzo ya urubani na wahandisi wa
ndege. Hata hivyo, Mamlaka inaendelea kushirikiana na vyuo vingine hapa nchini
kikiwemo Chuo cha Usafirishaji (NIT) ili kuhakikisha kwamba mafunzo hayo
yanatolewa hapa nchini.
Huduma za Viwanja vya Ndege
164.Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA)
imeendelea kuboresha miundombinu na huduma za viwanja vya ndege nchini ili
kuwezesha ndege kubwa na ndogo kutua na kuruka kwa usalama. Uboreshaji huo
unalenga kuviwezesha viwanja vya ndege nchini kutumika kwa majira yote ya mwaka
na kuvutia mashirika mengi zaidi ya ndege nchini ili kuongeza ushindani na
hivyo kupunguza gharama za usafiri wa Anga.
165.Mheshimiwa Spika, ujenzi wa jengo la tatu la abiria (Terminal III)
katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) unaendelea
kutekelezwa na unatarajiwa kukamilika Desemba 2017. Jengo hilo limeezekwa na
kazi zinazoendelea ni ujenzi wa kuta za ndani ya jengo, usimikaji wa madaraja
ya abiria kupandia/kushukia kwenye ndege, mifumo ya viyoyozi, miundombinu ya
umeme, mifumo ya maji safi na maji taka pamoja na mifumo ya zimamoto. Aidha,
ujenzi wa maegesho ya ndege umefikia hatua ya matabaka ya lami. Kukamilika kwa
jengo hilo kutaongeza uwezo wa kiwanja kuhudumia hadi abiria milioni 8.5 kwa
mwaka kutoka abiria milioni 2.5.
166.Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kusimamia uendeshaji na
uboreshaji wa Kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro ili kuhakikisha
kinakuwa bora na kuchangia katika ukuaji wa biashara za maua, mbogamboga,
matunda na utalii. Kazi za ukarabati wa kiwanja hiki zimekamilika kwa asilimia
70 na ujenzi unatarajiwa kukamilika Mei, 2017. Aidha, magari mawili mapya,
makubwa na ya kisasa ya zimamoto yalinunuliwa. Kukamilika kwa ukarabati wa KIA
kutaongeza uwezo wa barabara ya kuruka na kutua ndege kuhudumia ndege nyingi na
jengo la abiria kuwa na uwezo wa kuhudumia abiria milioni 1.2 kwa mwaka kutoka
abiria 500,000 wa sasa.
167.Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2016/2017, mradi wa ujenzi wa kiwanja
cha ndege cha Mwanza uliendelea kutekelezwa. Hadi kufikia Machi, 2017 hatua
iliyofikiwa ni kukamilika kwa kazi za kurefusha barabara ya kuruka na kutua
ndege kwa mita 500. Kazi zinazoendelea ni ujenzi wa jengo la kuongozea ndege,
ujenzi wa jengo la mizigo na maegesho ya ndege.
168. Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TAA inaendelea na awamu ya pili ya
ukarabati na uboreshaji wa Kiwanja cha Ndege cha Tabora. Kazi zinazotekelezwa
ni pamoja na ujenzi wa barabara ya pili ya kutua na kuruka ndege (secondary
runway), eneo la maegesho ya ndege (apron), barabara ya maungio (taxiway) kwa
kiwango cha lami, usimikaji wa mitambo ya kuongozea ndege (NavAids, DME na VOR)
na taa za barabara ya kurukia ndege (AGL). Kazi za ukarabati wa Kiwanja hiki
zilianza Septemba, 2016 na zinatarajiwa kukamilika Juni, 2017.
169. Mheshimiwa Spika, kuhusu ukarabati na upanuzi wa kiwanja cha ndege cha
Kigoma, Benki ya EIB ilitoa kibali (No Objetion) cha kutangaza upya zabuni ya
ukarabati Machi, 2017 kufuatia gharama za wazabuni kutokuwa shindani. Zabuni ya
marejeo inatarajiwa kutangazwa Mei, 2017. Kazi zitakazotekelezwa ni pamoja na
ujenzi wa Jengo la Abiria pamoja na miundombinu yake (maegesho ya ndege,
maegesho ya magari na barabara ya kuingia na kutoka), usimikaji wa taa na
mitambo ya kuongozea ndege, ujenzi wa uzio wa usalama na jengo la uchunguzi wa
hali ya hewa (OBS).
170. Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilika kwa ukarabati wa Kiwanja cha
Ndege cha Bukoba na kuanza kutumika, Serikali kupitia Mamlaka ya Viwanja vya
Ndege imekamilisha ujenzi wa shule mpya ya msingi katika eneo la Mafumbo.
Madhumuni ya ujenzi wa Shule hii ni kuweka mazingira mazuri ya utoaji wa huduma
za usafiri wa anga bila kuathiri utoaji elimu. Ujenzi wa shule hii ulikamilika
Aprili, 2017.
171. Mheshimiwa Spika, kazi nyingine zilizoendelea kutekelezwa katika mwaka
2016/17 ni pamoja na:
i.Usimikaji
wa taa za kuongozea ndege wakati wa kutua (PAPI) katika Kiwanja cha Ndege cha
Songwe ulikamilika Novemba, 2016;
ii.Kazi
ya kumpata Mkandarasi kwa ajili ya kuanza kazi za ukarabati na upanuzi wa
viwanja vya ndege vya Shinyanga na Sumbawanga zilikamilika Machi, 2017.
Ukarabati wa viwanja hivyo utaanza Mei, 2017;
iii.Nyaraka
za manunuzi ya Mtaalam Mwelekezi wa kazi ya kufanya mapitio ya upembuzi
yakinifu na usanifu wa miundombinu ya Kiwanja kipya cha Ndege cha Msalato
zimewasilishwa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) ili kupata “No Objection”.
Kazi hii inatarajiwa kuanza Agosti 2017;
iv.Kazi
za upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na kuandaa makabrasha ya zabuni kwa ajili
ya ukarabati na upanuzi wa viwanja vya ndege kumi na moja (11) vya Lake
Manyara, Musoma, Iringa, Tanga, Songea, Kilwa Masoko, Lindi, Moshi, Njombe,
Simiyu na Singida kwa kiwango cha lami. Kazi hizo zitakamilika Mei, 2017;
v.Kazi
za upembuzi yakinifu na usanifu wa awali kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa
Jengo la pili la abiria (TBII) katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha
Julius Nyerere imekamilika. Serikali inaendelea na majadiliano na Serikali ya
Ufaransa kwa ajili ya kupata fedha za utekelezaji wa mradi huo.
Huduma za Usafiri wa Anga
172.Mheshimiwa Spika, huduma za usafiri wa anga ndani na nje ya nchi zimeendelea kutolewa na
Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) pamoja na Kampuni za sekta binafsi zikiwemo
Precision Air, Fastjet, Auric na Coastal Air.
173.Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza azma yake ya kufufua
na kuboresha huduma za Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL) ili kusaidia kukuza
sekta nyingine za kiuchumi ikiwa ni pamoja na utalii, biashara, madini na
kilimo. Katika mwaka 2016/2017, Serikali iliingia mikataba ya ununuzi wa ndege
sita. Ndege mbili (2) aina ya Bombardier Dash 8 – Q400 zenye uwezo wa kubeba
abiria 76 kila moja ziliwasili nchini Septemba, 2016 na kuanza kazi Oktoba
2016. Ndege moja (1) aina ya Bombardier Dash 8 – Q400 itawasili nchini Julai,
2017; ndege mbili (2) aina ya Bombardier CS 300 zenye uwezo wa kubeba abiria
127 kila moja zitawasili nchini Juni, 2018 na ndege moja (1) ya masafa marefu
aina ya Boeing 787 Dreamliner yenye uwezo wa kubeba abiria 262 itawasili nchini
Julai, 2018.
174.Mheshimiwa Spika, ujio wa ndege hizo mbili aina ya Bombardier Dash 8 – Q400 pamoja na
ile iliyokuwepo aina ya Dash 8 - Q300 umeiwezesha ATCL kutoa huduma za uhakika
za usafiri wa anga katika maeneo ya Dar es Salaam, Mwanza, Kigoma, Arusha,
Kilimanjaro, Bukoba, Mbeya, Dodoma, Zanzibar na Moroni (Comoro). Kwa kutumia
ndege hizo tatu, ATCL inatarajia kupanua huduma zake katika maeneo ya Mtwara, Mpanda,
Songea na Tabora kuanzia mwezi Juni 2017. Safari za nchi jirani za Entebbe
(Uganda), Nairobi (Kenya), Bujumbura (Burundi) na Kigali (Rwanda) zitaanza
baada ya kupata ndege ya tatu ya aina ya Bombardier Dash 8 – Q400 Julai 2017.
Aidha, mara baada ya ndege aina ya Bombardier CS 300 kuwasili nchini, ATCL
itaanza safari za kwenda Afrika ya Magharibi, Afrika ya Kati, Afrika ya Kusini,
Mashariki ya Kati na India; na baadae kufanya safari za masafa marefu kwenda
China, Ulaya, na Marekani baada ya ndege ya Boeing 787 kuwasili.
175.Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha
Julai, 2016 hadi Machi, 2017, ATCL ilisafirisha abiria 47,510 ikilinganishwa na
abiria 32,434 waliosafirishwa katika kipindi kama hicho mwaka 2015/2016. Hii ni
sawa na ongezeko la asilimia 46. Ukuaji huu ulitokea kati ya Oktoba, 2016 na
Machi, 2017 baada ya upatikanaji wa ndege mbili mpya. Katika mwaka 2016/2017,
mifumo mipya na ya kisasa ya ukatishaji wa tiketi (reservation system),
udhibiti wa mapato (Revenue management system) na uhudumiaji wasafiri uwanjani
(Departure Control System) imefungwa. Aidha, ATCL imefungua kituo cha kisasa
cha huduma kwa wateja (call centre) ili kuondoa kero zitokanazo na matumizi ya
simu za kawaida katika kuhudumia wateja. Lengo ni kuongeza ubora wa huduma zake
kwa wateja. Kazi zinazoendelea kutekelezwa ni pamoja kuendelea na hatua za
kusafisha mizania ya ATCL; kuimarisha mifumo mbalimbali ya kielectroniki kwa
ajili ya uuzwaji wa tiketi za ndege na udhibiti wa mapato ya Kampuni; na
kuendeleza raslimali watu ili kuongeza ufanisi.
SEKTA YA UCHUKUZI Makadirio ya Matumizi ya Kawaida
na Bajeti ya Miradi ya Maendeleo
335.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa
fedha 2017/2018, Kampuni ya Ndege (ATCL) imetengewa shilingi milioni 500,000
kwa ajili ya kukamilisha malipo ya ununuzi wa ndege 3 ambapo ndege mbili (2) ni
za aina ya CS 300 zenye uwezo wa kubeba abiria 127 kila moja na ndege kubwa
moja (1) ya masafa marefu aina ya Boeing 787-8 Dreamliner yenye uwezo wa kubeba
abiria 262. Aidha, fedha hizo pia zitatumika kwa ajili ya gharama za bima,
mafunzo (marubani, wahandisi na wahudumu), gharama za kuanzia (start up cost)
pamoja na malipo ya awali ya ndege nyingine ya aina ya Boeing 787 (Dreamliner).
336.
Mheshimiwa Spika, Serikali
imeendelea kuboresha huduma zinazotolewa za Wakala wa 193 Ndege za Serikali.
Katika mwaka 2017/2018, Serikali imetenga Shilingi milioni 10,000 kwa ajili ya
kufanyia matengenezo ndege 4 za serikali ili kuhakikisha kuwa huduma ya usafiri
wa anga inatolewa kwa Viongozi Wakuu wa Kitaifa ni ya uhakika, salama na
inayokidhi viwango.
337.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali kupitia Mamlaka ya
Usafiri wa Anga imetenga fedha ili itatekeleza miradi mbalimbali ya kuboresha
shughuli za udhibiti wa usafiri wa anga. Miradi hiyo ni pamoja na: i. Kuboresha
miundombinu pamoja na huduma za usafiri wa anga nchini; ii. Kuendelea kutoa
huduma za uongozaji ndege kwenye eneo la Bahari ya Hindi hadi umbali wa nyuzi
44 mashariki; iii. Kuendelea na juhudi za kuendeleza ujenzi wa chuo kipya huko
Fukayose - Bagamoyo ili kuhakikisha chuo kinadahili wanafunzi wengi ambao
watahitimu katika nyanja ya usafiri wa anga; iv. Kufunga mtambo wa ILS
–Zanzibar; na v. Kununua na kufunga Rada nne (4) za kuongozea ndege za kiraia.
Kuipata hotuba kamili, bofya hapa http://www.mwtc.go.tz/uploads/publications/en1493281737-HOTUBA%20WUUM%202017-2018.pdf
0 Comments