Ticker

6/recent/ticker-posts

Header Ads Widget

Responsive Advertisement

Ajali ya Air India: Ripoti ya awali yasema usambazaji wa mafuta ya injini ulikatwa muda mfupi kabla ya ajali ya ndege ya Air India.

Ripoti ya awali imebaini kuwa ajali ya ndege ya Air India iliyotokea mwezi uliopita na kusababisha vifo vya watu 260 ilisababishwa na kukatwa kwa usambazaji wa mafuta kwenda kwenye injini.

Ndege hiyo yenye usajili VT-ANB ikifanya safari namba AI171, iliyokuwa ikielekea London ilikuwa imeondoka tu kwenye uwanja wa ndege wa Ahmedabad nchini India iliposhuka ghafla na kugonga majengo ya hosteli ya BJ Medical College, kisha kulipuka na kusambaratika huku mabawa, injini, magurudumu na sehemu nyingine zilitawanyika kwenye eneo hilo. Watu 241 waliokuwemo ndani ya ndege walifariki dunia, isipokuwa abiria mmoja tu aliyenusurika, na watu wengine 19 waliokuwepo ardhini waliuwawa pia.

Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Uchunguzi wa Ajali za Ndege la India (AAIB), swichi za udhibiti wa mafuta (Fuel Control Switches) katika chumba cha marubani wa ndege hiyo aina ya Boeing 787 Dreamliner zilikuwa zimezimwa, jambo lililosababisha injini kukosa mafuta.


Wachunguzi waliweza kupata taarifa kutoka kwenye vinasa sauti vya ndege vinavyojulikana kama “black box,” (EAFR) zikiwemo saa 49 za data za safari na saa mbili za mazungumzo ndani ya chumba cha marubani, ikiwa ni pamoja na kumbukumbu za ajali hiyo.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, ndege hiyo ilikuwa imefikia mwendo wa anga wa kasi ya 180 knots wakati swichi za kukata mafuta za injini zote mbili zilipobadilishwa kutoka nafasi ya “RUN” hadi “CUTOFF” moja baada ya nyingine kwa tofauti ya sekunde moja tu.

“Katika rekodi ya sauti ya marubani, rubani mmoja alisikika akiuliza kwa mshangao kwa nini mwenzake amekata mafuta. Rubani mwenzake alijibu kuwa hakufanya hivyo,” inasomeka ripoti hiyo.

Muda mfupi baadaye, swichi hizo zilirejeshwa kwenye nafasi zake sahihi, na injini zilikuwa katika mchakato wa kuwashwa tena wakati ajali ilipotokea.

Katika ndege ya 787, swichi za kukata mafuta ziko kati ya viti vya marubani wawili, mara moja nyuma ya vishikizo vya kuongeza kasi ya ndege (throttles). Swichi hizo zinalindwa pembeni kwa upau wa chuma na zina kifaa cha kufunga kilichoundwa mahsusi kuzuia kukatwa kwa bahati mbaya.

 “Wakati swichi za udhibiti wa mafuta zinapohamishwa kutoka CUTOFF hadi RUN ndege ikiwa angani, kila injini ina mfumo wa kiotomatiki wa kudhibiti kuwashwa tena na kurejesha nguvu, kwa kusimamia mchakato wa kuwasha moto na kuingiza mafuta,” inasema ripoti hiyo.

Sekunde chache baada ya injini kujaribu kuwashwa tena injini moja iligoma kuwaka, rubani mmoja alisikika akipaza sauti, “MAYDAY MAYDAY MAYDAY.” Msimamizi wa mnara wa uwanja wa ndege aliita namba ya utambulisho ya ndege hiyo, lakini hakupata majibu, na alitazama ndege ikiporomoka kwa mbali.



Rubani mkuu wa safari hiyo alikuwa na umri wa miaka 56 na alikuwa na zaidi ya saa 15,000 za urubani katika maisha yake. Rubani msaidizi alikuwa mwanaume mwenye umri wa miaka 32, akiwa na zaidi ya saa 3,400 za kurusha ndege.

Wachunguzi pia walibaini kuwa mipangilio ya vifaa vilivyopatikana kwenye mabaki ya ndege ilikuwa ya kawaida kwa safari ya kuruka. Mafuta ya ndege yalichunguzwa na kubainika kuwa ya viwango vinavyokubalika, na hakuna dalili za idadi kubwa ya ndege wa mwituni waliokuwa karibu na njia ya ndege hiyo.

Uzito wa ndege wakati wa kuruka ulikuwa ndani ya viwango vinavyokubalika, na hakukuwa na “mizigo hatari” ndani ya ndege hiyo. Wachunguzi walibaini mabawa ya ndege yalikuwa kwenye nafasi ya nyuzi tano (5 degrees), ambayo ni sahihi kwa kuruka, na swichi ya magurudumu ilikuwa kwenye nafasi ya kushuka.

Ripoti ilisema kuwa injini ya kushoto ilisimikwa kwenye ndege hiyo tarehe 26 Machi, na injini ya kulia ilisimikwa tarehe 1 Mei.

Safari ya ndege ya Air India 171 ilianza kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Sardar Vallabhbhai Patel mjini Ahmedabad, katika jimbo la Gujarat, India, tarehe 12 Juni. Boeing 787-8 Dreamliner hiyo ilikuwa ikielekea Uwanja wa Ndege wa London Gatwick, Uingereza, na ilitarajiwa kutua saa 12:25 jioni kwa saa za huko.




Air India ilisema kuwa kulikuwa na abiria na wahudumu 242 ndani ya ndege hiyo, wakiwemo raia 169 wa India, Waingereza 53, Wareno 7 na Mkanada 1.

Mbali na waliokuwa ndani ya ndege, watu kadhaa waliokuwa ardhini waliuawa wakati ndege hiyo ilipogonga hosteli ya Hospitali na Chuo cha Matibabu cha BJ.

Ajali hiyo ilisababisha vifo vya jumla ya watu 260, kwa mujibu wa ripoti hiyo. Baadhi ya waliokufa ardhini walikuwa waliogongwa na ndege hiyo ilipogonga hosteli.

Air India ilikiri kupokea ripoti hiyo na ikasema itaendelea kushirikiana na mamlaka katika uchunguzi huo.

“Air India inatoa pole na kusimama pamoja na familia na wote walioathirika na ajali ya AI171,” shirika hilo liliandika kwenye X siku ya Jumamosi (kwa saa za huko). “Tunaendelea kuomboleza vifo hivyo na tumejitoa kikamilifu kutoa msaada katika kipindi hiki kigumu.”

 

Post a Comment

0 Comments