Bw Barnett
alifanya kazi katika kampuni kubwa ya utengenezaji ndege ya Marekani “Boeing” kwa
miaka 32, (miongo mitatu) hadi alipostaafu mwaka wa 2017 kwa misingi ya afya.
Kuanzia 2010,
alifanya kazi kama meneja wa ubora katika kiwanda cha North Charleston
akitengeneza 787 Dreamliner, ndege ya kisasa inayotumiwa hasa kwenye njia za
masafa marefu.
Mnamo mwaka wa
2019, Bw Barnett alitoa taarifa kwamba wafanyakazi walio kwenye shinikizo kubwa
la kazi wamekuwa wakiweka kwa makusudi sehemu zisizo na ubora kwenye ndege
wakati wa uzalishaji / uundaji.
Pia alisema
amegundua shida kubwa na mifumo ya oksijeni, ambayo inaweza kumaanisha barakoa
moja kati ya nne ya kupumua haitafanya kazi wakati wa dharura, itapokuwa inahitajika.
Alisema mara
baada ya kuanza kazi huko South Carolina aliingiwa na wasiwasi kwamba msukumo
wa kukamilisha kujengwa au kuundwa kwa ndege mpya ulimaanisha mchakato wa kuunganisha
vifaa vya ndege uliharakishwa na hivyo usalama kuathiriwa, jambo ambalo kampuni hiyo ya Boeing ilikanusha.
Baadaye alitoa
taarifa kwamba wafanyakazi walishindwa kufuata taratibu zilizokusudiwa kufuatilia (kudhibiti) kwa ukaribu vifaa / sehemu za ndege mpaka kiwandani zinapotengenezwa, hivyo kuruhusu sehemu za ndege zenye kasoro kutoonekana / kutoweka.
Alisema katika
baadhi ya matukio, sehemu za ndege zilizo chini ya kiwango zimetolewa hata
kwenye mapipa ya vifaa vinavyosubiri kuharibiwa kwa kukosa ubora, na vikarejeshwa
kuwekwa kwenye ndege zinazoendelea kujengwa ili kuzuia kuchelewa kwa uzalishaji.
Pia alidai kuwa
vipimo kwenye mifumo ya dharura ya oksijeni iliyopaswa kuwekwa kwenye Boeing 787
vilionyesha kiwango cha kushindwa kwa asilimia ishirini na tano (25%),
ikimaanisha kuwa mfumo mmoja kati ya minne ungeweza kushindwa kupatikana wakati
wa dharura.
Bw Barnett
alisema alikuwa amewaarifu wasimamizi kuhusu wasiwasi wake, lakini hakuna hatua
iliyochukuliwa.
Boeing ilikanusha
madai yake. Hata hivyo, ukaguzi wa wa mwaka 2017 wa mdhibiti wa usafiri wa anga
Marekani,FAA, ulizingatia na kutilia maanani baadhi ya taarifa za Bw Barnett.
Katika ukaguzi
huo FAA iligundua kuwa ngalau sehemu 53 "zisizo sawa" za ndege
hazikuweza kujulikana mahali zilipo kiwandani hapo, na kwamba zilizingatiwa
kuwa zimepotea. Boeing iliamriwa kuchukua hatua za kurekebisha.
Kuhusu suala la
mitungi ya oksijeni, kampuni hiyo ilisema kuwa mnamo 2017 "imegundua chupa
za oksijeni zilizopokelewa kutoka kwa mtoaji ambazo hazikuwa zikitumwa
ipasavyo". Lakini ilikanusha kuwa yoyote kati yao ililikuwa imefungwa
kwenye ndege.
Baada ya
kustaafu, alijikita katika kuchukua hatua za kisheria dhidi ya kampuni hiyo.
Aliishutumu kwa
kudhalilisha wadhifa wake na kutatiza kazi yake kwa sababu ya masuala aliyoyaibua
– mashtaka ambayo yaliyokataliwa na Boeing.
Wakati wa kifo
chake, Bw Barnett alikuwa Charleston kwa mahojiano ya kisheria yaliyohusishwa
na kesi hiyo.
Wiki iliyopita,
alitoa maelezo rasmi ambapo alihojiwa na mawakili wa Boeing, kabla ya kuhojiwa
na wakili wake mwenyewe.
Alikuwa
anatazamiwa kuhojiwa zaidi siku ya Jumamosi. Aliposhindwa kutokea katika
mahojiano, ukaguzi ukafanywa katika hoteli aliyokuwa amefikia.
Baadaye alikutwa
amekufa kwenye gari lake kwenye maegesho ya hoteli.
Ofisi ya
mchunguzi wa maiti wa kaunti ya Charleston ilithibitisha kifo chake siku ya
Jumatatu. Ilisema mzee huyo wa miaka 62 alikufa kutokana na jeraha la
"kujiumiza" mnamo Machi 9 na polisi walikuwa wanachunguza.
Kwa mujibu wa habari, wakili wake alieleza kifo chake kuwa cha kusikitisha.
Katika taarifa yake, Boeing ilisema: "Tumehuzunishwa na kifo cha Bw. Barnett, na mawazo yetu
yako kwa familia yake na marafiki."
Kifo chake
kinakuja wakati viwango vya uzalishaji katika kampuni ya Boeing na wasambazaji wake muhimu
Spirit Aerosystems viko chini ya uchunguzi mkali.
Hii inafuatia kisa cha mapema Januari wakati mlango wa kutokea wa dharura ambao haujatumika ulipofyatua ndege mpya kabisa aina ya Boeing 737 Max muda mfupi baada ya kupaa kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Portland. Ripoti ya awali kutoka kwa Bodi ya Kitaifa ya Usalama wa Usafiri ya Marekani ilipendekeza kwamba boliti nne muhimu, zilizoundwa kushikilia mlango kwa usalama, hazikuwa zimefungwa.
Wiki iliyopita,
FAA ilisema ukaguzi wa wiki sita wa kampuni hiyo umepata "matukio mengi
ambapo kampuni inadaiwa kushindwa kufuata mahitaji ya udhibiti wa ubora wa
utengenezaji".
Vyanzo vya habari; mitandao, bbc.
0 Comments